Tanzania logo

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

BARAZA DOGO LA WAFANYAKAZI WIZARA YA MAMBO YA NDANI YA NCHI LAKUTANA KUPITIA MPANGO WA BAJETI KWA MWAKA 2023/24 NA TAARIFA YA UTEKELEZAJI KUANZIA JULAI 2022-JANUARI 2023.



Baraza dogo la Wafanyakazi  Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi limekutana na kupitia mpango wa bajeti wa mwaka 2023/2024 pamoja na taarifa ya utekelezaji wa mpango na bajeti kuanzia Julai 2022 –Januari 2023 kwa mwaka wa fedha 2022/2023.

Akizungumza kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi, Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Rasilimali watu Miriam P. Mbaga ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza hilo Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, amesema kuwa matarajio ya Baraza hilo ni kuhakikisha kuwa Watumishi wanashiriki na kutoa maoni, ushauri na mapendekezo yao ipasavyo ili kuboresha mazingira ya utendaji kazi na kuboresha maslahi ya Watumishi na kufanikisha ufanisi na utendaji bora wa Wizara kwa Wananchi.

Akifungua Baraza hilo Katibu Tawala Mkoa wa Dodoma Dk Fatuma Mganga ameliomba Baraza hilo kuhakikisha kuwa wanasimamia na kuhamasisha utekelezaji wa majukumu kuzingatia  kiapo cha ahadi ya uadilifu na kuweza kutumia rasilimali zilizopo katika kufanikisha utekelezaji wa majukumu.

“Rai yangu kwenu tutumie mikutano ya Baraza la Wafanyakazi kujadili mambo yatakayoimarisha utendaji kazi ili kufikia malengo ya Wizara na Serikali kwa ujumla. Tujue kwamba tunawatumikia Watanzania wenzetu. Panapoibuka changamoto na malalamiko ndani ya Wizara tujue kwamba kuna mmoja wetu ambaye hajatekeleza majukumu yake vizuri. Ni kazi ya Baraza kukumbushana ili utendaji wetu wa kazi uwe na tija.” alisema Dk Mganga.

Aliendelea kusema kuwa,  “Kama tunavyofahamu bajeti ni nyenzo muhimu katika utekelezaji wa mipango ili kufanikisha utekelezaji wa majukumu na pia kufikia katika muda uliopangwa na kutoa matokeo tarajiwa. Wakati wote rasilimali huwa haitoshi lakini inapaswa kutumia rasilimali zilizopo kufanya utekelezaji wa majukumu kulingana na vipaumbele.”

Katika hatua nyingine  Mganga amehimiza uwepo wa mahusiano mema kati ya  Watumishi kwa Watumishi na Watumishi na Wakurugenzi wa Idara mbalimbali kwani mahusiano ndio mtaji katika kufanikisha utendaji kazi. Aidha, amewasisitiza Viongozi kuacha ubinafsi na kusimamia maslahi ya wanaowaongoza kwa kuhakikisha  kuwa kila  Mtumishi anapata anachostahili ili kuwa na mahusiano bora katika eneo la kazi.

Wakizungumza na kutoa tathmini ya mkutano wa Baraza hilo la Wafanyakazi baadhi ya Watumishi wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi akiwemo Francis Rubert ambaye pia ni  Katibu wa Baraza dogo la Wafanyakazi Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi amesema kuwa mkutano huo umekuwa ni wa manufaa makubwa kwao kwani kupitia mkutano wa baraza hilo mambo mengi yameweza kuelekezwa kwa ajili ya kuboresha ufanisi katika utendaji kazi ikiwa ni pamoja na kukumbushwa wajibu wa utendaji kazi kwa kuzingatia maadili ya Utumishi wa Umma.

Boaz Mwazyunga Katibu wa TUGHE tawi la Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi amesema kuwa Baraza limekuwa likisaidia utekelezaji wa masuala mbalimbali ya Kiutumishi ndani ya Wizara na masuala hayo  yamekuwa yakizingatiwa kwa uwazi na kumekuwa na  mgawanyo wa matumizi kwa kuwashirikisha Watumishi na kuhimiza usawa miongoni mwa Watumishi wa Wizara.

Ikumbukwe kuwa mkutano huo wa Baraza unalengo la kupitia mpango wa bajeti wa mwaka 2023/2024 pamoja na taarifa ya utekelezaji wa mpango na bajeti kuanzia Julai 2022 –Januari 2023 kwa mwaka wa fedha 2022/2023.