Tanzania logo

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

BILIONI1.4 ZATUMIKA KUJENGA OFISI ZA KAMANDA WA POLISI MKOA WA MARA



Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi (Mb) Mhe. Jumanne Sagini amefanya ziara ya kutembelea na kukagua Mradi wa Ujenzi wa Jengo la Ofisi ya Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara katika eneo la Manispaa ya Musoma wenye thamani ya shilingi Bilioni 1.4.

Akizungumza baada ya kukagua wa Mradi huo Mhe. Sagini amesema kuwa, kukamilika kwa Mradi huo utaipa heshima na hadhi Ofisi ya Kamanda wa Polisi kwani kila Kitengo kitakuwa na Ofisi yake tofauti na ilivyo kuwa sasa.

"Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni sikivu na nimearifiwa kuwa, fedha za awamu ya pili na tatu tayari zimetoka hivyo basi nimuombe mkandarasi kukamilisha ujenzi kama inavyoelekeza ili ofisi ianze kutumika." Alisema

Kwa upande wake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara ACP Salim Morcase, amemshukuru Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi na Wizara kwa ufuatiliaji wa karibu wa Mradi wa Ujenzi wa Jengo la Ofisi ya Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara.

“Sisi kama Jeshi la Polisi kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchi tunatoa shukurani zetu za dhati kwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na kwako kwa ufuatiliaji wa karibu wa Mradi wa Ujenzi wa Jengo letu”. Alisema ACP Morcase

Aidha, amebainisha kuwa, Mradi huo mpaka sasa umefikia asilimia 92 na ulianza kutekelezwa Novemba 18, 2021 na unakadiriwa kumalizika mwishoni mwa mwezi Disemba mwaka 2023.