Tanzania logo

Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

SAGINI AAGIZA KUFUTIWA LESENI MADEREVA WANAOKIUKA SHERIA BARABARANI



Naibu Waziri wa mambo ya ndani ya nchi, Jumanne Sagini amemuagiza Kamanda wa Kikosi cha usalama Barabarani nchini pamoja na vyombo vya usimamizi wa sheria barabarani kuwachukulia hatua ikiwezekana kuwafutia Leseni madereva wote wanaokiuka sheria ili kupunguza vifo vinavyotokana na uzembe wa madereva.

Sagini ametoa agizo hilo mara baada ya kufika eneo iliyotokea ajali na kutembelea majeruhi katika ajali iliyohusisha gari la Ally’s lililokuwa linatoka Dar es Salaam kwenda Mwanza kugonga Treni ya mizigo katika makutano ya barabara na Reli maeneo ya Manyoni Mkoani Singida.

“Nimuelekeze pia Kamanda wa Usalama barabarani Taifa kupitia idara zake chini ya RTO’s, wawe wakali kuondoa huruma kwa watu wanaovunja sheria kama hawa, vyombo vyote vya usimamizi wa sheria za barabarani ikiwemo LATRA na Polisi lazima tuchukue hatua madhubuti kusaidia Watanzania wasipoteze maisha kama haya ambayo yametokea ni uzembe mkubwa wa Dereva wetu”

“Kitendo cha basi kugonga kichwa cha treni mpaka kikahama kikaacha njia ya Treni inaonyesha dhairi kwamba dereva alikuwa kwenye mwendo mkali sana, jambo hili linahuzunisha na mara zote tumekuwa tukiwakumbusha madereva na wamiliki wa magari, madereva wao wazingatie sheria za usalama barabarani na dereva huyu wa kampuni ya Ally’s sio mgeni barabara hii kwamba unapofika Manyoni baada ya kituo kuna Reli halafu round about, ambapo kwa maeneo yote anapaswa kwenda mwendo mdogo”, amesema Jumanne Sagini Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi.

Aidha mmoja Kati ya majeruhi ameomba mamlaka ya usafirishaji iweze kuzingatia juu ya vidhibiti mwendo kwenye Magari ili kupunguza ajali za barabarani.

“Sijui kama kuna utaalam wa ku monitor speed za Magari kwa sababu abiria hawapo conscious muda wote hawawezi kujua kama gari linaweza kuwa linakimbia kwa speed, kwa hiyo kama kuna namna ambayo Magari yanaweza yakadhibitiwa," ameeleza Majeruhi